MABADILIKO YA HALI YA ANGA, MAJONZI KWA BINADAMU

 Labda nikisema dalili za kiama zimeanza kuonekana nitazidi kuumiza mitima ya waja hapa duniani, ila kusema ukweli ni kwamba watu wanazidi kuumia na kuteseka kila uchao kutokana na mabadiliko ya ghafla ya hali ya anga.Ni mara ngapi tumesikia vifo vya watu kutokana na makali ya njaa ambayo yamechangiwa na tabianchi?

Hapo awali enzi za babu za babu zetu mambo yalikuwa nywee! Yani asili hizo maisha yalikuwa matamu kama asali sikwambii halua, watu wa jadi hizo waliishi maisha ya raha na starehe huku wasijue bei ya vyakula ni nini.Maisha yao yalikuwa shwari kama ya peponi ila sasa,ni vilio na simanzi kila pembe ya taifa letu tukufu la Kenya.

Walumbi husema,msiba wa kujitakia hauna kilio lakini huu wa sasa uko na kilio kikubwa sana.Kila jambo mtu analonuia kulifanya ni lazima kama ibada kukadiria matokeo yake yatakuwaje kabla kuamua kulifanya.Shida nyingi tunazopitia tumezichangia sisi wenyewe,tumekumbatia kikiki mfumo mpya wa kitekinolojia ambao umetuathiri sisi binafsi vibaya.

Jambo la kwanza lililoharibu hali ya hewa ni kujengwa kwa viwanda.Ijapokuwa viwanda vingi vina umuhimu mkubwa hapa nchini lakini badhii ya viwanda hivyo hutema mawingu ya moshi yanayotokana na uzalishaji wa bidhaa ambapo moshi huo hupaa angani na kuchanganyikana na mawingu ya mvua mwishowe huwa sumu hatari kwa binadamu,wanyama na mimea.Fauka ya hayo moshi huo hutatiza ozoni inayozuilia miale ya jua kugonga ardhini mwishowe majani ya mimea kukosa hata umande wa asubuhi.

Pia ukataji wa miti kwa nia ya kuchoma mkaa,umeleta balaa kubwa katika maisha ya sasa.Miti ambayo sote twajua fika kuwa ni kivutio cha mvua lakini na jambo hilo tumelifumbia macho na kuyatia maskio yetu nta na kusahau kabisa umuhimu wa miti.Kutokana na ukataji huo,mvua imekata kabisa kunyesha katika nchi yetu.Visa vingi vya njaa vimeripotiwa katika Kaunti tofauti tofauti ikiwemo Mandera,Wajir,Kilifi,Marsabit,West Pokot na Baringo ambazo ni baadhi tu ya Kaunti za taifa la Kenya zinazogugunwa na jinamizi la ukame.Ni juzi tu ambapo eneobunge la Ganze katika ya Kaunti ya Kilifi liliangaziwa kwenye vyombo vya habari baada ya wenyeji kula matunda ya msituni ili kushtaki njaa iliyowatafuna matumbo yao kutokana.Hii yote imetokana na kiangazi kikali kama nyuki kilichovamia sehemu hiyo.

Minghairi hayo wawindaji haramu huchoma misitu kiholela mwishowe kusababisha donda sugu la jangwa lisilokuwa na tiba milele na kuhatarisha maisha ya wanayama,wadudu na mimea.Vilevile mfumo mpya wa uzalishaji wa chakula umeathiri afya za binadamu,wanyama wadudu na mimea.Kutokana na unyunyuziaji wa mbolea ambazo zingine zina sumu,zimechangia sana kuangamia kwa viumbe wengi.Pia urushaji na uchomaji ovyo taka hususan vifaa vya plastiki pia umesababisha machafuko na kuharibu hali ya hewa kwa asilimia kubwa,mfano jaa la Mwakirunge katika Kaunti ya Mombasa linanuka fe! Huku mawingu ya moshi yakikotana na kuchanganyika na mawingu,jamani,tunaelekea wapi?

Waswahili husema kinga ni bora kuliko tiba,kwa hivyo tunafaa kujua kuwa mabadiliko haya ya anga au hewa ni sisi sisi tuliochangia.Tunafaa kuwa mstari wa mbele kulinda na kutunza mazingira yetu,tupande miti kwa wingi na tujiepushe na mambo ambayo yatatuletea shida chungu nzima baadae,tusisahau kuwa heri kuziba ufa kuliko kuziba ukuta.


MOHAMMED KAZUNGU kutoka Chuo Kikuu cha Kiufundi cha Mombasa (TUM) katika kitengo cha Habari na Mawasiliano

Mwandishi wa makala haya.


Comments

  1. Hii ni Kazi nzuri kabisa na ujumbe mzito, hongera

    ReplyDelete
  2. Hongera sana ,Mungu akubarikie πŸ‘πŸ€²

    ReplyDelete
  3. Good workπŸ‘

    ReplyDelete
  4. Nzuri mkaliπŸ”₯πŸ”₯πŸ”₯

    ReplyDelete
  5. A Very nice article

    ReplyDelete
  6. Congratulations 🎊 πŸ‘

    ReplyDelete

Post a Comment

Popular posts from this blog

HALUWA SI TAMU TENA VYUONI

MALEZI

BAADA YA DHIKI FARAJA